Jumapili , 18th Oct , 2020

Uongozi wa Mtibwa Sugar umethibitisha kuwa kocha Zuberi Katwila, amejiuzulu nafasi yake kuanzia leo Oktoba 18, 2020 baada ya kuwasilisha barua.

Zuberi Katwila

Akizungumza na East Africa Radio, Afisa Sheria na Utawala, Sabri Aboubakar amesema uamuzi wa Zuberi kuondoka klabuni hapo ni wake binafsi na wao kama uongozi wamebariki baada ya pande zote mbili kuridhia.

Sababu za kujiuzulu kwa kocha huyo hazijawekwa wazi kufuatia makubaliano ya pande hizo mbili kukubaliana kuwa ni siri.

Katwila amejiuzulu ikiwa ni siku chache baada ya Mtibwa kupoteza mchezo wa tatu mfululizo wa ligi kuu na mara ya mwisho walinyukwa 2-0 na Gwambina.

Katwila amedumu katika klabu ya Mtibwa tangu mwaka 1999 akiwa mchezaji kabla ya kugeukia ukocha kwa miaka 8, huku mitatu katika hiyo alikua kocha mkuu wa wakatamiwa hao.

Mikoba yake kwa sasa imeachwa kwa Vicent Barnabas ambaye alikua msaidizi wake tangu kuanza kwa msimu.