Jumanne , 7th Jun , 2016

Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limeridhia uchaguzi wa Yanga uendeshwe na klabu yenyewe na utafanyika Juni 11, mwaka huu - jambo ambalo ni ushindi kwa wanachama wa klabu hiyo inayopatikana maeneo ya jangwani jijini Dar es Salaam.

Ofisi za Makao Makuu ya Shirikisho la Soka nchini TFF.

Hayo yamefikiwa katika kikao cha pamoja baina ya Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi na uongozi wa Yanga chini ya Makamu Mwenyekiti anayemaliza muda wake, Clement Sanga.

Sanga ambaye amechukua fomu za kutetea nafasi yake, aliambatana na Katibu Mkuu wa klabu hiyo, Baraka Deusdedit kwa ajili ya kujadili mustakabali wa uchaguzi wa Yanga ambao uliingia katika mvutano na TFF pamoja na BMT.

"Maamuzi yaliyotoka ni kwamba, uchaguzi wa Yanga umebarikiwa kuendelea kama ulivyopangwa na kamati ya uchaguzi ya Yanga kwamba utafanyika June 11, 2016 chini ya uangalizi wa kamati ya uchaguzi ya TFF," amesema Afisa Habari wa TFF, Alfred Lucas leo Dar es Salaam.

Lucas amesema kwamba wagombea wa nafasi mbalimbali kwenye uchaguzi huo ambao walichukua fomu TFF, kikao kimeamua kiwarudishe kamati ya uchaguzi ya Yanga kuendelea na taratibu zilizopo za uchaguzi endapo wanakidhi vigezo vya uchaguzi vya kamati ya uchaguzi ya Yanga.

Mvutano uliibuka kuhusu uchaguzi wa Yanga SC kiasi cha kuwaacha njia panda wanachama wa klabu hiyo, wakiwa hawajui washike lipi, baada ya TFF kutangaza na kuendesha mchakato wa uchaguzi wa klabu hiyo - wakati huo huo klabu hiyo nayo ikitangaza na kuendesha mchakato wake huo yenyewe.

Yanga ilisema uchaguzi wake utafanyika Juni 11 na na TFF ikasema utafanyika Juni 25. Na wote na zote zikaanza kugawa fomu za kugombea wiki iliyopita.

Waliochukua fomu TFF ni Aaron Nyanda, Titus Osoro wanaowania nafasi ya Makamu Mwenyekiti, Paschal Laizer, Edgar Chibula, Mohammed Mattaka, Mchafu Ahmed Chakoma, Bakari Malima ‘Jembe Ulaya’ Omari Said kutoka Zanzibar wanaowania Ujumbe wa Kamati ya Utendaji, wakati miongoni mwa waliochukua fomu Yanga ni pamoja na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF, Ayoub Nyenzi.

Wakati mvutano huo, ukiendelea uongozi wa Yanga ukaibua tuhuma za TFF kwa kushirikiana na Kamati yake ya Uchaguzi chini ya Mwenyekiti, Wakili Alloyce Komba kupanga njama za kuhujumu uchaguzi huo.

Kwa tuhuma hizo, mwishoni mwa wiki Wakili Komba alitangaza kujitoa kusimamia mchakato wa uchaguzi wa Yanga.