Jumapili , 25th Jun , 2017

Kikosi cha Taifa Stars leo kinatarajiwa kutupa karata yake ya kwanza kuwania ubingwa wa mashindano ya Kombe la Cosafa kwa kuikabili Malawi katika mechi ya Kundi A itakayopigwa leo jijini Johanesburg, Afrika Kusini.

Taifa Stars inashiriki kwa mara ya tatu michuano hiyo ya kila mwaka katika Ukanda wa nchi za Kusini mwa Afrika.

"Tunataka kufanya vizuri katika mashindano haya, lakini pia ni muhimu kuimarisha kikosi chetu kwa ajili ya michuano ya CHAN ambayo iko mbele yetu," amesema Kocha wa Stars Salum Mayanga.

Baada ya mechi ya leo, Stars itashuka tena dimbani keshokutwa kuikaribisha Angola na itamaliza mechi za hatua ya makundi kwa kuvaana na Mauritius ifikapo Juni 29, mwaka huu.

Katika michuano ya CHAN, Stars itacheza mechi yake ya kwanza nyumbani dhidi ya Rwanda (Amavubi) Julai 14, mwaka huu na Julai 21 itaifuata jijini Kigali kwa ajili ya mechi ya marudiano.