Jumamosi , 10th Dec , 2016

Timu za Simba SC na Azam FC zimefanikiwa kuingia katika hatua ya Fainali ya Michuano ya Vijana wenye umri chini ya miaka 20 zinazotarajiwa kuchezwa hapo kesho katika Uwanja wa Chamazi jijini Dar es salaam

Vijana wa Azam wakishangilia ushindi wa jana

 

Simba SC na Azam FC zote zimeingia katika hatua ya fainali kwa mikwaju ya penati hapo jana Uwanja wa Chamazi jijini Dar es salaam.

Timu ya Simba imefanikiwa kuingia fainali baada ya kuitoa kwa penalti 8-7 Stand United ya Shinyanga ambapo katika mikwaju tisa, Simba walipoteza mmoja na Stand wakapoteza miwili baada ya dakika 120 za timu hizo kufungana bao 1-1.

Awali, Simba ndiyo waliotangulia kupata bao lililofungwa na Hussein Hamisi dakika ya 19 kwa shuti kali baada ya pasi ya Rashid Juma, kabla ya Stand kusawazisha kupitia kwa Adam Salamba dakika ya 53 kwa mkwaju wa penalti baada ya beki wa Simba kuunawa mpira kwenye boksi.

Kwa upande wa Azam FC, imetinga fainali baada ya kuichapa Mtibwa Sugar kwa mikwaju ya penati 4-2 kwenye mchezo wa nusu fainali, kufuatia sare ya bila kufungana ndani ya dakika 90 na 30 za nyongeza.