Jumapili , 15th Mei , 2016

Timu ya Taifa ya vijana wenye umri chini ya miaka 17 Serengeti Boys, ambayo ipo India kwa ajili ya michuano maalumu ya soka ya Kimataifa kwa vijana (AIFF Youth Cup 2016 U-16) iliyoandaliwa na Shirikisho la Soka nchini humo imeanza vema michuano hiyo.

Timu za Taifa za Vijana za Tanzania na Marekani zikiwa kwenye Uwanja wa Tilak Maidan, Vasco, Goa India kabla ya kuanza kwa mchezo.

Kikosi cha timu ya taifa ya vijana chini ya miaka 17, cha Serengeti Boys kimefanikiwa kuanza michuano ya vijana ya nchini India kwa sare ya bao 1-1.

Serengeti Boys ambayo ilionyesha soka safi hasa kipindi cha kwanza kinamalizika ilikuwa ikiwa na sare ya bao 1-1.

Kwa mujibu wa shuhuda, mechi hiyo ilikuwa ngumu kipindi cha pili mwanzoni. Lakini kipindi cha pili mwishoni Serengeti Boys wakashambulia zaidi ingawa hawakufanikiwa kufunga.

Mechi inayofuata ni Alhamisi ijayo na Serengeti Boys watashuka uwanjani kuwavaa Korea Kusini katika mechi yao ya pili.

Mechi za michuano hiyo zote zinapigwa kwenye Uwanja wa Tilak Maidan, Vasco, Goa nchini humo.

Fainali ya michuano hiyo itachezwa Mei 25 ambapo kabla ya mchezo wa fainali, utachezwa mchezo wa mshindi wa tatu katika uwanja huo huo Tilak Maidan, Vasco, Goa nchini India.

AIFF kimeandaa mashindano ya vijana wenye umri chini ya miaka 17, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kikosi chao kwa ajili ya Fainali za Kombe la Dunia kwa Vijana zitakazofanyika nchini humo mwaka 2017.