Jumatano , 1st Dec , 2021

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Profesa Joyce Ndalichako amesema kuwa Sera, Sheria, Kanuni, Taratibu na Miongozo vitasimamiwa ipasavyo ili kuimarisha ufundishaji na ujifunzaji wa michezo shuleni na katika Vyuo vya Ualimu.

Mgeni rasmi, Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Pauline Gekul akipita kukagua timu mbalimbali zinazoshiriki mashindano ya UMISAVUTA yanayoendelea mkoani Mtwara

Hayo yamesemwa kwa niaba yake mapema wiki hii, mkoani Mtwara na Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Pauline Gekul katika muendelezo wa mashindano ya Umoja wa Michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu Tanzania (UMISAVUTA) yanayoendelea mkoani humo hadi Desemba 5, 2021.

Amesema Rais Samia Suluhu alitoa maelekezo ya kuboresha mitaala na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa katika nyakati tofauti ameagiza kutekelezwa kwa ufundishaji wa masomo ya sanaa na michezo, hivyo Wizara inaendelea kutekeleza maagizo hayo ili kufikia azma ya Serikali ya kuhakikisha vipawa vya wanamichezo na Sanaa vinakuzwa kuanzia shuleni na pia Taifa linakuwa na wananchi wenye nguvu na afya njema kuweza kulitumikia Taifa.

Aidha, katika hatua nyingine Naibu Waziri Gekul amewataka washiriki wote wa mashindano hayo kuhakikisha wanachukua tahadhari zote za maambukizi ya ugonjwa wa Uviko-19 katika kipindi chote cha mashindano hayo, na kuwahimiza kupata chanjo ya ugonjwa huo.

Awali, Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. James Mdoe alisema lengo la mashindano hayo ni kukuza na kuendeleza vipaji kwa walimu tarajali ili nao waweze kwenda kukuza vipaji vya wanafunzi katika michezo na sanaa.

Aidha Naibu Katibu Mkuu huyo amemuhakikishia mgeni rasmi kuwa Wizara itahakikisha mashindano hayo yatafanyika kwa nidhamu na maadili hadi yanapofikia tamati.

Naye Mwenyekiti wa Walimu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali Tanzania Bara, Mwl. Dorothy Mhaiki amesema mashindano hayo yamehusisha wanachuo 665 kutoka vyuo 36 vya ualimu vikiwemo 35 vya Serikali na kimoja binafsi.

Timu za mpira wa miguu kutoka Kanda ya Ziwa na Kanda ya Kati ndizo zilizofungua dimba la mashindano hayo ambapo timu ya Kanda ya Ziwa iliibuka na ushindi wa mabao 3-0.