Ijumaa , 26th Mei , 2017

Kiungo wa kimataifa wa Rwanda anayekipiga katika klabu ya Dar es Salaam Young Africans (Yanga) Haruna Niyonzima amefunguka na kusema yeye atawaaga wana Yanga kwa amani wakati huo utakapofika kwa kuwa ameishi nao kwa muda mrefu kwa upendo na amani.

Haruna Niyonzima

Niyonzima alisema hayo baada ya tetesi kuzuka kuwa msimu ujao hatakuwa tena Yanga na kuwa atakwenda kukipiga katika klabu nyingine ndipo hapo aliposema kwa sasa hayupo kwenye nafasi nzuri ya kulizungumzia jambo hilo ila kama litatokea basi ataagana vizuri na klabu hiyo ambayo ameichezea kwa muda mrefu.

"Hilo suala siwezi kulizungumzia sana unajua Yanga ni timu ambayo nimekaa nayo na ninaiheshimu, ni timu ambayo nimeweza kudumu kwa miaka mingi hivyo naamini nikija kupata fursa ya kutoka au kuondoka kwenda sehemu nyingine naamini wana Yanga nitawaaga kwa amani na vizuri kabisa lakini kwa sasa siwezi kuzungumza chochote" alisema Niyonzima 

Katika msimu wa ligi ambao umemalizika wiki iliyopita Haruna Niyonzima aliyanyakua tuzo ya mchezaji bora wa kigeni.