Ijumaa , 10th Nov , 2017

Katibu Mkuu wa Yanga, Boniface Mkwasa amesisitiza kuwa ni lazima wampe adhabu na onyo kali mshambuliaji wao Mzimbabwe, Donald Ngoma kwa utovu wa nidhamu wa kutoweka bila taarifa

Mkwasa amesema hayo, wakati akizungumza na Kipenga ya East Afrika Radio jana baada ya kuulizwa swali katika mahojiano maalumu kuhusiana na timu ya Yanga kuelekea michezo ijayo ya ligi kuu.

Japo Yanga wenyewe kupitia kwa katibu mkuu wake Mkwasa wamekiri kutofahamu chochote kwa sasa juu ya nini kimemsibu mchezaji huyo wala wapi aliko, lakini taarifa za kidukuzi ambazo Kipenga imezinyaka zinasema kuwa, mshambuliaji huyo aliondoka nchini kimya kimya na kurejea nyumbani kwao Zimbabwe bila ya kutoa taarifa kwa viongozi wake. 

Mkwasa amesema, hawana taarifa za kuondoka kwa mshambuliaji huyo aliyekuwepo nje ya uwanja kwa muda wa wiki tatu na nusu kutokana na kusumbuliwa na majeraha ya goti.

“Hatuna taarifa za kuondoka kwa Ngoma na kama ameondoka basi atakuwa kafanya makosa kwani hakutoa taarifa kwa uongozi.

“Hivyo, kama akirejea nchini na kujiunga na klabu ni lazima tumchukulie hatua za kinidhamu ikiwemo adhabu kwa kitendo alichokifanya,” amesema Mkwasa.