Jumatano , 1st Dec , 2021

Kikosi cha Kinondoni Municipal Council FC, kimeanza rasmi maandalizi kuelekea katika mchezo mwingine wa Ligi Kuu ya NBC soka Tanzania Bara dhidi ya Geita utakaopigwa siku ya Jumapili ya Disemba 5 katika Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.

Hayo yamebainishwa na Christina Mwagala ambaye ni Ofisa Habari na Mawasiliano wa KMC FC.

KMC FC ambao ni wenyeji wa mchezo huo, kikosi kimeanza kujifua mapema tangu Jumanne, Novemba 30,2021 ikiwa ni baada ya kurejea jijini Dar es Salaam siku ya Jumapili kutoka jijini Mbeya ambapo ilikuwa kwenye mchezo dhidi ya Mbeya City uliomalizika kwa sare ya magoli mawili kwa mawili.

Katika maandalizi hayo, timu hiyo ya Manispaa ya Kinondoni chini ya Kocha Mkuu John Simkoko inakwenda kujiimarisha zaidi ili kuhakikisha kuwa katika mchezo huo ambao itakuwa mwenyeji inabakiza alama tatu muhimu.

KMC FC inahitaji kupata matokeo mazuri katika uwanja wa nyumbani licha ya kuwa inakutana na timu ambayo kimsingi ni bora na yenye ushindani lakini maandalizi ambayo yanaenda kufanyika yataleta matokeo chanya.

"Kwenye mchezo wetu uliopita hatujapata kile ambacho tulikuwa tunakihitaji kwa maana ya ushindi, lakini matokeo hayo hayatuvunji moyo badala yake yametupa changamoto ya kuendelea kujiweka vizuri zaidi kwenye mchezo ambao tutakuwa nyumbani.

"Kwetu sisi kama timu tunahitaji kufanya vizuri kwenye michezo yetu ambayo tunacheza na kwamba bado tunaendelea kupambana ili kufanya vizuri zaidi katika michezo yote iliyopo mbele yetu," ameeleza Ofisa huyo.

Mpaka Sasa kwenye msimamo wa NBC Premier league, watoza ushuru wa Kindononi, KMC wanashikilia nafasi ya 14 wakiwa na Alama 6.