Jumatatu , 5th Apr , 2021

Mratibu wa mapambano ya bondia Antony Joshua Eddie Hearn, amethibitisha kuwa bondia huyo ameaanza maandalizi ya kujiandaa na pambano dhidi ya Tyson Fury, lakini pia tarehe na sehemu pambano hilo litakapo fanyika itathibitishwa wiki ijayo.

Antony Joshua akimshambulia mpizani wake kwenye moja ya mapambano yake

Ilithibitishwa kuwa mabondia hao wawili Tyson Fury na AJ wamesaini mkataba wa makubaliano wa kupigana mkataba unaoonyesha utakuwa na mapambano mawili, wenye thamani ya pesa za Uingereza pauni milioni 200 ambazo ni zaidi ya bilion 643 kwa pesa za kitanzania.

Eddie Hearn amesema AJ amejipanga kwenda kuweka kambi yake ya mazoezi kwenye chuo cha michezo kilichopo mjini Sheffield, sambamba na mkufunzi wake Rob McCracken. Mratibu huyo akaweka wazi kuwa mpaka wiki ijayo mipango yote juu ya pambano hilo litafanyika wapi na lini itakuwa imekamilika.

Mabondia hawa wawili wanashikilia mikanda yote ya uzito wa juu, Antony Joshua anashikilia mikanda minne ya uzito wa juu ambayo ni WBA, IBF, WBO na IBO wakati Tyson Fury anashikilia mkanda wa WBC. Kwa kigezo cha mabondia hawa kutoka Uingereza kushikilia mikanda yote ya uzito wa juu, Pambano hilo linatajwa kuwa kubwa kwenye historia ya mchezo wa masumbwi Uingereza.