Alhamisi , 12th Nov , 2020

Mkuu wa Mkoa wa Dar Es Salaam Abubakar Kunenge amesema atalifanyia kazi tukio la mama mmoja ambaye alisimulia kupotea kwa mtoto wake wa kiume kisha kumkuta kwenye choo akiwa amefariki.

Mkuu wa Mkoa wa Dar Es Salaam Abubakar Kunenge

Mama huyo alijitambulisha kwa jina la Mariam Aly mkazi wa Tandale kwa Mtoogole alitoa taarifa hiyo kupitia show ya DADAZ ya East Africa TV, ambapo amesema mwanaye anaitwa Fahad ana umri wa mwaka mmoja na miezi 10 na alipotea kwa mazingira ya kutatanisha.

Mariam Aly akaendelea kusema tukio hilo lilitokea siku ya Oktoba 26, ila baada ya kupita siku 3 walikuta mwili wa mtoto wake upo kwenye shimo la choo akiwa amefariki na alidai jirani yake ndiyo alimtupa mwanaye kwenye choo hicho.

Aidha ameongeza kusema kesi ikafika kituo cha polisi lakini kwa bahati mbaya hakupata ushirikiano kutoka kwa polisi hao ambao walimjibu afanye upepelezi mwenyewe kuhusu tukio la mtoto wake.

Taarifa hiyo imemfikia Mkuu wa Mkoa wa Dar Es Salaam Abubakar Kunenge, ambapo baada ya kuona  video fupi aliyo-post mtangazaji wa DADAZ Maye Kidoti kupitia ukurasa wa Instagram aka-comment kuwa "ahsante kwa taarifa, nalifanyia kazi".