Jumapili , 13th Aug , 2017

Mke wa msanii Roma, Nancy Ibrahim amesema kulingana na matatizo ambayo waliyapitia na mumewe, asingeweza kuachia kazi mpya, kwa jinsi ambavyo ilimuathiri kisaikolojia.

Msanii Roma

Akizungumza kwenye kipindi cha Friday Night Live kinachorushwa na East Africa Television, Nancy amesema kwa jinsi ambavyo walikuwa kwenye wakati mgumu miezi miwili nyuma, Roma asingeweza kuachia kazi yoyote kwani hata uwezo wamkuandika aliuwa hana.

"Mwezi wa tano hivi au wa sita ungemwambia atoe asingeweza, kwa sababu kichwa nacho kilikuwa hakiko sawa, hata kuandika ni ngumu, kwa sasa hivi tunamshukuru Mungu maisha yanaendelea, tumerudi nyumbani, mtoto anaenda shule", alisema Nancy.

Nancy aliendela kusema kuwa kitendo hiko kiliwafanya wawe karibu zaidi kwa kumjua Mungu na kusali, kwani walikuwa na uoga wa hali ya juu.

"Matatizo yametubadilisha wote kiujumla sio Roma peke yake, matatizo yametupa uoga wa maisha, matatizo yametufanya tumemjua zaidi Mungu, unajua saa nyingine unapitishwa katika jambo ili ujifunze kitu fulani, pia yametufanya tunamjua zaidi Mungu, tunasali sana, kingine ndio hicho yani, uoga sana sana, tunavyozidi kusali uoga unapungua maisha yanaendelea tunafanya shughuli zetu zinaendela kama kawaida", alisema Nancy.