Jumapili , 16th Oct , 2016

Msanii Ney wa Mitego amesema maisha aliyokuwa anaishi yamemjengea ujasiri na kujiamini hata pasipostahili, na ndicho kitu kikubwa kilichomfanya aweze kufanya muziki wa tofauti hata asipoungwa mkono na watu.

Ney wa Mitego

Akizungumza kwenye Planet Bongo ya East Africa Radio, Ney wa Mitego amesema maisha hayo yalimfanya asimuogope mtu yeyeite hata kama kamzidi umri, lakini ili mradi ameridhisha nafsi yake.

"Life style ambayo niliishi ilinijengea ujasiri wa kipuuzi ambao ninao, nilikuwa najiamini kupita maelezo, kabla sijaleta rap yangu ya maisha niliyokuwa naishi kwenye muziki, nilikuwaga mtu ambaye hata nikikaa tu maskani ukinikera mi nitakwambia, uwe mkubwa, uwe mdogo uwe baba uwe mama, ntakwambia tu hapo hapo alafu roho yangu inakuwa safi, sitojali we utalipokea vipi, nilikuwa mtu wa kujichanganya sana", alisema Ney wa Mitego.

Ney wa Mitego aliendelea kusema kuwa kitendo hicho ndicho kilichomsababisha awe anaandika nyimbo tofauti ambazo zinakuwa gumzo, hata asipopata suport kutoka kwa watu.

"Naweza nikafanya muziki wa tofauti na wenzangu, najua watu watashangaa, may be wanaweza wasisuport lakini acha nifanye, so niliamua, ndiyo maana wimbo wangu wa kwanza nilimzungumzia baba yangu, nilimzungumzia mama yangu ijapokuwa tafsiri yake ilikuwa tofauti, kwa wanawake ambao wanatupa watoto", alisema Ney wa Mitego.