Jumatatu , 25th Sep , 2017

Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe amesema wizara yake imefuta mashindano ya Miss Tanzania kwa sababu yaligubikwa na ubabaishaji mwingi katika uendeshaji wake.

Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe.

Dkt. Mwakyembe ameeleza hayo baada ya kupita takribani miezi mitatu tokea alipokabidhiwa zawadi yake Miss Tanzania 2016/2017, Diana Edward ambayo ilizua maneno mengi katika mitandao ya kijamii wakidai zawadi hiyo ya gari waliyompatia Miss huyo ilikuwa imechakaa na kupewa nje ya wakati na kushusha hadhi ya mashindano hayo pamoja na kuvunja moyo kwa watu ambao walikuwa na lengo la kushiriki katika mashindano mengine yajayo.

"Mimi na wizara yangu tuna mikakati tofauti kabisa, tungependa vitu vyote tunavyo vianzisha viwe na muendelezo na siyo vianzishwe leo keshokutwa vimekatika. Niwatolee mfano kidogo tulikuwa na Miss Tanzania hapa chini lakini nimepiga marufuku kwa sababu ya uswahili mwingi ambao mimi siwezi kuukubali nikiwa kiongozi wa hii wizara, kwa hiyo nimewakatalia wote hakuna cha miss Tanzania", amesema Dkt. Mwakyembe.

Pamoja na hayo, Dkt. Mwakyembe ameendelea kwa kusema "Endapo watataka kuendesha hayo mashindano nitahitaji zawadi ya mshindi wa kwanza kama ni gari iletwe ofisini kwangu niione na waniachie funguo yake pia zawadi ya mshindi wa pili hivyo hivyo ndipo nikaporuhusu. Maana kila mwaka zawadi ya mshindi wa kwanza imekuwa ikisumbua kutolewa kwa muhusika. Sasa huo mchezo hapana, hatuwezi kuona ukiendelea, ubabaishaji siyo kwa Tanzania ya leo"

Kwa upande mwingine, Dkt. Mwakyembe amesema sasa anachokifanya ni kukaa chini na baadhi ya wadau wa masuala ya 'fashion' ili waweze kuyaboresha mashindano hayo yaweze kuwa bora na kufanyika kila mwaka bila ya kuwa na ubabaishaji.