Jumapili , 18th Oct , 2020

Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Aboubakar Kunenge, amefanya ziara ya kushtukiza usiku wa kuamkia leo Oktoba 18, 2020, kwenye Ujenzi wa Machinjio ya kisasa Vingunguti, Soko la Kisutu na Stendi ya kisasa Mbezi Louis na kubaini kwenye Machinjio ya Vingunguti na Soko la Kisutu, wakandarasi

Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam Aboubakar Kunenge

hawafanyi kazi usiku na mchana kama alivyowataka.

Kunenge amesema kukiukwa kwa agizo la kufanya kazi usiku na Mchana kumepelekea miradi hiyo kushindwa kukamilika ndani muda uliopangwa na kuleta kero kwa wananchi.

Kutokana ukiukwaji wa maagizo yayo RC Kunenge ametoa maagizo matatu mazito kwa Manispaa ya Ilala ikiwemo kuhakikisha Mkandarasi anapigwa faini kwa kushindwa kukamilisha ujenzi ndani ya muda kwa mujibu wa mkataba, Kumchukulia hatua za kinidhamu Msimamizi wa Mradi pamoja na kumuwajibisha Mhandisi Manispaa hiyo kwa kushindwa kusimamia kazi yake.

Aidha RC Kunenge amemuelekeza Mkurugenzi wa Manispaa hiyo kumpatia mapendekezo ya jinsi gani watakamilisha miradi hiyo kwa haraka ili iweze kuwa msaada kwa wananchi.

Ukiacha Soko la Kisutu na Machinjio ya Vingunguti, kwenye ujenzi wa Stand Mpya ya Mbezi Louis RC Kunenge amekuta kazi inafanyika usiku na Mchana, ikiwa ni utekelezaji wa Agizo la Rais Dkt. John Magufuli alilotoa wakati wa hafla ya uwekaji jiwe la msingi na kuagiza Mradi ukamilike kabla ya mwishoni mwa mwezi Novemba.

RC Kunenge amesema leo Oktoba 18 jumla ya Makontena 13 yenye Vifaa vya Ujenzi wa Stand ya Mbezi yaliyokuwa yamekwama bandarini yataanza kutoka baada ya kufanya mazungumzo na viongozi wa Wizara na Mamlaka ya Mapato TRA.