Jumapili , 22nd Nov , 2020

Katibu Mkuu, Wizara ya Afya Idara Kuu ya Maendelo ya Jamii, Dkt. John Jingu, amesema ujenzi wa nyumba bora katika jamii utasaidia wananchi kuwa na makazi bora na kuondokana na vitendo vya ukatili ambavyo wakati mwingine huanzia katika ngazi ya familia.

Katibu Mkuu Wizara ya Afya- Idara Kuu ya Maendelo ya Jamii Dkt. John Jingu akionesha Mwongozo ya uboreshaji makazi

Dkt. Jingu ameyasema hayo katka kijiji cha Ilalangulu, kilichopo katika Halmshauri ya Mpwimbwe, mkoani Katavi , wakati akihamasisha Kampeni ya kuboresha Makazi inayoendelea katika mikoa mbalimbali nchini ambapo amesema, wizara inatekeleza mipango ya maendeleo ambayo imepewa kipaumbele katika Ilani ya CCM ya mwaka 2020-2025 ambayo imeweka wazi umuhimu wa makazi bora kwa taifa lenye afya.

“Wizara inahamashisha wananchi kuboresha makazi yao kwa kujiunga katika vikundi ili kupata mikopo itakayowawezesha kuboresha makazi”. amesema Dkt. Jingu 

Ameongeza kuwa na makazi bora ni maendeleo ya jamii kwani makazi bora yanasaidia familia kuwa na Amani na utulivu katika ustawi wao kwa ujumla, “Ukiwa hauna nyumba bora unakaribisha wageni wengine kama mende, kunguni, panya na wadudu hatarishi kagtika makazi wanaoondoa amani katika familia” alisema Dkt. Jingu

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mpwimbwe Godfrey Nkuba amesema Halmashauri hiyo imefika asilimia 70 ya makazi bora katika vijiji na Kata zilizopo.

Naye mmoja wa wananchi aliyeboresha makazi yake kwa kutumia kipato chake na mikopo cha vikundi Elizabeth Nyanda amesema kuwa mpango wa Taifa wa kunusuru kaya masikini (TASAF) umemsaidia kupata mtaji wa biashara iliyomuwezesha kujenga nyumba mbili za kisasa na kutoka katika nyumba ya tope na nyasi.

Wizara ya Afya- Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii inaendesha Kampeni maalum ya kuhamasisha jamii kuboresha makazi yao ikiwa na kauli mbiu isemayo: “Piga Kazi Boresha Makazi”