Alhamisi , 14th Jan , 2016

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amekutana na kufanya mazungumzo na mabalozi wawili kutoka nchi za Qatar na Kuwait.

Waziri Mkuu, Kassim Majliwa akizungumza na balozi wa Qatar nchini, Mhe. Abdallah Jassim al Maadadi ofisini kwake jijini Dar es salaam

Akizungumza kwa nyakati tofauti na mabalozi hao ofisini kwake ,Magogoni jijini Dar es salaam, Waziri Mkuu amewashukuru mabalozi hao kwa pongezi walizokuja kumpatia, pamoja na namna ambavyo nchi zao zimekua zikisaidia Tanzania, ambapo ameahidi kuendeleza ushirikiano mzuri baina ya Tanzania na nchi zao.

Kwa upande wake, Balozi wa Qatar, Abdallah Jassim al Maadad amesema Serikali yake itaendelea kuisaidia Tanzania katika maeneo yote ambayo Qatar imepiga hatua kubwa na inaweza kutoa msaada kwa Tanzania.

Amesema Kuwait iko tayari kuwekeza nchini katika sekta ya kilimo, kwa vile ardhi ya Tanzania ni yenye rutuba na inafaa kwa shughuli za kilimo. Aidha, ametaja sekta nyingine ambazo wangependa kuwekeza ni pamoja na sekta ya uvuvi na viwanda.

Naye, Balozi wa Kuwait, Jasem Al Najem ambaye amekuja kujitambulisha kwa Waziri Mkuu, amesema nchi yake kupitia ‘Kuwait fund’ iko tayari kuendelea kuisaidia Tanzania katika miradi mbalimbali ya maendeleo.