Jumatatu , 13th Apr , 2015

Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato nchini Tanzania Rished Bade amewataka watumishi TRA kuzingatia maadili ya kazi na hatosita kuwachukulia hatua wale watakaoenda kinyume ikiwa ni pamoja na kuomba na kupokea rushwa.

Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato nchini Tanzania Rished Bade.

Kamishna Bade amesema hayo leo wakati akifungua mafunzo ya mwaka mmoja kwa wafanyakazi wapya 150 ambao watapata mafunzo ya kukusanya kodi kisasa na kiuweledi pamoja na kujifunza mbinu za kisasa za kukusanya kodi ambazo hutumiwa na nchi zilizoendelea duniani.

Kwa mujibu wa Kamishna Bade, kazi ya ukusanyaji kodi una vishawishi vingi hususani rushwa kutoka kwa wafanyabiashara wanaokwepa au kutaka kupunguza kiwango cha kodi, hivyo ni jukumu la watumishi hao wapya kutambua changamoto hiyo na kujiepusha nayo.

Amesema katika kuzingatia mafunzo wanayoyatoa yanakidhi mahitaji ya kazi ya ukusanyaji kodi, kamishna Bade amesema muda wa masomo umeongezwa kutoka miezi mitatu iliyokwepo awali, hadi mwaka kipindi cha mwaka mmoja.

Kwa Upande wake Mkuu wa Chuo cha Kodi Profesa Isaya Jairo amewataka wafanyakazi hao kusoma kwa bidii ili kuja kuisaidia nchi yetu kukusanya kodi kwa maendeleo ya Taifa na kujiepusha na vishawishi vya rushwa na kufanya kazi kwa bidii.

Kwa Upande wao wafanyakazi hao wamesema watafaidika sana na mafunzo hayo kwani watafundishwa masomo ya kukabiliana na vishawishi vya rushwa pamoja na mbinu kisasa za kukusanya kodi.