Jumatano , 16th Sep , 2020

Watu wanne wamefikishwa mbele ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kkisutu Jijini Dar es Salaam wakikabiliwa na mashitaka ya uhujumu uchumi, ikiwemo kujihusisha na usafirishaji wa dawa za kulevya aina ya heroin kilo 51.47.

Washitakiwa hao ni Ernest Michael Semayoga, Salum Jongo, Amini Sekibo na Tatu Nassoro ambao wamesomewa mashitaka hayo mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Cassian Matembele na mawakili wa serikali Paul Kadushi, Wankyo Simon na Benson Mwaitenda.

Imedaiwa Mahakamani hapo kwamba kati ya mwezi Septemba mwakam 2020 katika Mtaa wa Veterinary Temeke mkoa wa Dar es Salaam walijihusisha na kuwa na dawa za kulevya aina ya heroin kilo 51.47.

Katika shitaka la pili washitakiwa wote kwa pamoja kati ya Septemba 1 na 8 mwaka 2020 katika Jiji la wa Dar es Salaam walitenda kosa la utakatishaji fedha haramu kwa kujipatia kwa njia ya udanganyifu fedha za kitanzania shilingi milioni 62,370,000, fedha za Msumbiji 7,370, Fedha ya Kenya shilingi 400, na magari manane ya aina tofauti.

Katika shitaka la tatu ndani na nje ya mkoa wa Dar es Salaam kati ya Septemba 1 na 8 mwaka 2020 inadaiwa washitakiwa walitenda kosa la kuongoza genge la uhalifu kwa kusafirisha dawa za kulevya aia ya heroine kilo 51.47.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Septemba 30 na washitakiwa wataendelea kusota rumande kutokana na makosa hayo kuwa hayana dhamana.