Ijumaa , 14th Nov , 2014

Serikali ya Tanzania imetakiwa kuanzisha mahakama maalumu itakayokuwa na jukumu la kushughulikia masuala na kesi zinazohusu uwekezaji.

Katibu Mkuu wa chama cha Upinzani cha CCK nchini Tanzania Renatus Muhabi.

Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam na vyama vitano visivyo na uwakilishi bungeni kupitia kwa mwenyekiti wa kamati maalum ya maatibu wakuu wa vyama hivyo Bw. Renatus Muhabi.

Kwa mujibu wa Muhabi, mahakama ya uwekezaji itakuwa na jukumu la kushughulikia kwa haraka kesi na mashauri yote yanayohusu uwekezaji, ambapo ametolea mfano wa sakata la IPTL na tuhuma za ufisadi katika akaunti ya Tegeta Escrow ni moja ya mambo ambayo yangeweza kushughulikiwa ipasavyo na mahakama hiyo.

Aidha Muhabin ameongeza kuwa Watanzania hawaridhishwi na dana dana inayoendelea kutokea katika sakata la IPTL na kwamba kuna haja ya waziri Mkuu Mizengo Pinda kupima utendaji wake hasa hatua alizochukua katika kushughulikia sakata la IPTL.

Muhabi amesema kuwa akiwa kama msimamizi mkuu wa shughuli za serikali, Waziri Mkuu Mizengo Pinda alitakwa awe amechukua maamuzi ya kuepusha madhara yanayojitokeza kutokana na sakata la IPTL, hasa namna nchi hivi sasa inavyokosa misaada ya wahisani kutokana na tuhuma za ufisadi zinazohusiana na sakata hilo.