Alhamisi , 26th Mei , 2016

Wanawake wajawazito na watoto wenye umri wa miezi 9 mkoani Mtwara wanatarajiwa kunufaika na mpango wa Chandarua Kliniki unaotekelezwa na mradi wa kimataifa wa Vectorworks, wenye lengo la kuongeza upatikanaji na matumizi ya vyandarua vyenye viuatilifu

(Picha na Maktaba)

Akizungumza na waandishi wa habari katika utambulisho wa mpango huo katika Hospitali ya rufaa ya Ligula, Mganga mkuu wa mkoa wa Mtwara, Dkt. Wedson Sichalwe, amesema walengwa watapatiwa vyandarua hivyo bila malipo yoyote wakati wakuudhuria Kliniki.

Kwa upande wake, Afisa habari elimu na mawasiliano kutoka wizara ya afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto, Theresia Shirima, amesema kiwango cha maambukizi ya malaria kitaifa kwa sasa ni asilimia tisa ambapo lengo ni kufikia asilimia moja ifikapo mwaka 2020.

Mpango wa Chandarua Kliniki unaosimamiwa na wizara ya afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto kupitia mpango wa taifa wa kudhibiti malaria, unatarajiwa kuzinduliwa Mei 28 katika uwanja wa Mashujaa mkoani Mtwara huku mgeni rasmi akitarajiwa kuwa mkuu wa mkoa wa Mtwara, Halima Dendego.