Jumanne , 23rd Mei , 2017

Watu watatu ambao ni wanafunzi wa Shule ya Msingi Butwa mkoani Geita wamefariki dunia baada ya mtumbwi waliokuwa wakisafiria kuzama katika Ziwa Victoria, mkoani Geita.

Muonekano wa ziwa Victoria (Picha: Maktaba)

Kamanda wa Polisi Mkoani Geita amesema tukio hilo lilitokea jana majira ya saa 10 jioni wakati wanafunzi hao walipokuwa wakivuka maji kwa kutumia mitumbwi miwili wakitoka shuleni katika kisiwa cha Isimacheli  kurudi majumbani kwao katika kisiwa cha Lulegea.

Amesema wanafunzi hao jumla walikuwa 24 ambao walijigawa kwa kupanda wanafunzi 12 katika kila mtumbwi ambapo mtumbwi wa kwanza ulifanikiwa kuvuka salama, lakini mtumbwi wa pili ulielemewa mawimbi na hatimaye kuzama.

Amesema kwamba kabla mtumbwi huo haujazama, nahodha wa mtumbwi huo baada ya kuona anaelemewa aliamua kurudi nyuma ili aurudishe ufukweni lakini wakati akijaribu kurudi mtumbwi ulizidiwa na kuzama ambapo wanafunzi 9 wote wa kiume walinusurika baada ya kufanikiwa kuogelea huku watatu ambao wote ni wa kike wakipoteza maisha.

Amewataja waliofariki dunia kuwa ni pamoja na Kumbuka Bahati (13) mwanafunzi wa darasa la 3, Anastazia Mwita mwanafunzi wa darasa la 3 na Sophia Lusala mwanafunzi wa darasa la Kwanza.

Amesema mwili wa mwanafunzi mmoja ulipatikana jana majira ya jioni na miili miwili imepatikana leo ikiwa imeharibika vibaya

Jeshi hilo linamshikilia nahodha wa mtumbwi huo anayefahamika kwa jina la Hulugu Kayalenda na uchunguzi bado unaendelea.