Jumatano , 11th Feb , 2015

Jeshi la polisi wilayani Mvomero mkoani Morogoro limezuia maandamano ya wakulima wa miwa Turiani waliotaka kuandamana kwa lengo la kulalamikia kiwanda cha Mtibwa kushindwa kulipa madeni yao kwa muda mrefu.

Wakizungumza kwa jazba wakulima hao wakiwemo wazee wamesema hawaoni sababu ya jeshi la polisi wakiwa na silaha kuwazuia kufanya maandamano ya kudai haki yao kwani ni muda mrefu wanalalamikia kiwanda bila majibu.

Ingawa wamepewa muda kuwa kufikia tarehe 20 mwezi huu watakuwa wamelipwa, wamesema endapo hawatatimiziwa ahadi hiyo wananchi watalazimika kuhamishia makazi yao kiwandani hadi kieleweke.
 
Diwani wa kata ya Mtibwa Lukas Mwakambaya na ambaye alihojiwa na jeshi la polisi kwa saa kadhaa katika kituo cha polisi Mtibwa akizungumza na wananchi amesema jeshi la polsi limezuia maandamnao hayo kutokana na kukosa kibali.

Amesema haokuona sababu ya jeshi la polisi kutumia silaha na kuweka utepe kuzua wakulima  wasiingie kiwandani kudai haki yao kwani walifanya biashara na kiwanda na wana haki ya kulipwa jasho lao.
 
Naye meneja wa kiwanda cha Mtibwa Sugar Ahmed Yahaya amekiri  madai ya wakulima hao ni ya msingi na ameshindwa kulipa kwa wakati kutokana na kuharibika kwa soko la sukari la ndani baada ya kupata hasara kufuatia na uingizaji holela wa sukari bila ushuru ambapo ameahidi tarehe 20 mwezi huu atafanya malipo yote ya wakulima.