Jumamosi , 10th Mei , 2014

Jamii wa wafugaji kutoka Wilaya ya Narock nchini Kenya wamezipongeza jamii za Wamasai na Wasonjo kwa hatua ya makubaliano ya kumaliza uhasama ambao umekuwepo kati yao kwa muda mrefu.

Hatua  ya  wananchi  wa  jamii  ya  Wamasai  na  Wasonjo   ya kukubaliana  kumaliza  tofauti  zao  kwa njia  ya  mazungumzo  na   kufichua  mtandao   unaoingiza  silaha  za  kivita  katika  maeneo  yao  imeungwa  mkono  na  wafugaji   wa  wilaya  ya  Narock  nchini  kenya.

Wafugaji hao wamepongeza hatua hiyo kwakuwa silaha hizo  hutumika   kuua wananchi   wasio  na  hatia na  wameahidi  kutoa  ushirikiano  wa  hali  na  mali.

Kiongozi  wa  mila  wa  wafugaji  wa wilaya  ya    Narock   Bw  Nicholaus Kiripesi  amesema  muafaka  wa  wamasai   na  wasonjo  uliofikiwa  unahitaji  kuungwa  mkono  sio  tu  na  wananchi  wa  jamii  hizo  bali  hata  wa  jamii  nyingine na pia viongozi wa  kada  mbalimbali.

Amesema  kama  wafugaji hao wa  Tanzania  wakiweza  kudumisha  makubaliano  waliyofikia  ya kuondoa  tofauti  zao,   suala  la  kukabiliana  na  mtandao  wa  watu  wanaoingiza  silaha  litakuwa  rahisi  na  ni jambo linalowezekana.

Kwa  upande  wake  mwenyekiti  wa  kamati ya usuluhishi  wa  mgogoro  wa  Wamasai  na  Wasonjo  Bw  Rafael  Long'oi   na  mkuu   wa  wilaya  ya  Ngorongoro  Bw  Elias  Wawalali  wamewataka  wananchi  wa  pande zote mbili  kuunga mkono  jitihada  za  wazee  wa  mila  za  kudumisha  makubaliano  hayo  kwa  kuendelea  kuwafichua  wanaomiliki  silaha  na  kwamba  watakaosalimisha  hawatachukuliwa  hatua  yoyote.

Kwa  mara ya kwanza  katika  historia  ya  jamii  za  wamasai  na  wasonjo,   wananchi  wakiwemo  vijana   wa  jamii  hizo   walikula  na  kucheza  pamoja  hali inayoonesha  kumaliza  tofauti  zao.