Alhamisi , 25th Aug , 2016

Kumeibuka mtindo mpya wa ukwepaji kodi unaofanywa na baadhi ya wafanyabiashara wakubwa wasio waaminifu, ambao huuza bidhaa zao kwa mtindo unaotumiwa na wafanyabiashara ndogo ndogo maarufu kama wamachinga.

Baadhi ya machinga maeneo ya Kariakoo Jijini Dar es salaam

Mtindo huo umekuwa ukifanywa kwa kutandaza na kuuza bidhaa zao pembezoni mwa barabara na katika maeneo yasiyo rasmi.

Ukwepaji kodi huo umeshika kasi hivi karibuni, siku chache baada ya Rais Dkt John Pombe Magufuli, kutoa amri ya kutonyanyaswa kwa wafanyabiashara ndogo ndogo, unyanyasaji uliokuwa ukidaiwa kufanywa na viongozi wa halmashauri za wilaya na miji nchini, hatua inayoelezwa kuwa ni matumizi mabaya ya nafuu hiyo iliyotolewa na Rais.

East Africa Radio imewasiliana na Mkurugenzi wa Habari wa Jumuiya Wafanyabiashara nchini JWT, Bw. Stephen Chamle, ambaye ameonesha kusikitishwa na ukwepaji kodi huo, kwa maelezo kuwa mbali ya kuikosesha serikali mapato, umekuwa ukiathiri pia ushindani kwa kuwepo makundi mawili ya wafanyabiashara, moja likiwa ni lile linalolipa kodi na lingine linalofanya biashara kiujanja ujanja.