Jumanne , 14th Oct , 2014

Nchi wahisani wa maendeleo kwa Tanzania, zimetoa ufafanuzi kuhusiana na hatua ya hivi karibuni ambapo nchi hizo zimezuia kwa muda shilingi bilioni 937 ambazo ni misaada yao ya kibajeti kwa Tanzania.

Balozi wa Finland nchini Tanzania na Mwenyekiti wa Wadau wa Maendeleo Bi. Sinikka Antila.

Katika maelezo yao, wahisani hao wamesema fedha hizo zitatolewa mara tu ofisi ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa serikali CAG, itakapokamilisha ripoti ya uchunguzi kuhusiana na sakata la malipo ya zaidi ya shilingi bilioni 200, zilizotolewa kwa kampuni ya kufua umeme ya IPTL.

Mwenyekiti wa wadau hao wa maendeleo, Balozi wa Finland nchini Bi. Sinikka Antila, amesema hayo katika mahojiano Maalumu yaliyofanyika ofisini kwake mtaa wa Mirambo jijini Dar es Salaam, na kuweka wazi kuwa wadau wa maendeleo wamekuwa wakifuatilia kwa umakini mkubwa sakata hilo, kutokana na kuhusisha tuhuma za ubadhirifu wa kiasi kikubwa cha pesa za umma.

Katika mahojiano hayo yaliyofanyika ofisini kwake mtaa wa Mirambo jijini Dar es Salaam, Balozi Antila amesema anaamini ofisi ya CAG itaharakisha pamoja na kufanya uchunguzi huo katika mazingira huru na ya haki, ili kila mdau aweze kuchukua maamuzi sahihi yanayotokana na ripoti ya uchunguzi ulio huru.

Hata hivyo kiasi kilichotolewa na wahisani hao mpaka sasa ni dola za Marekani milioni 69, takribani fedha za Tanzania shilingi bilioni 110, na kwamba kusitishwa kwa misaada hiyo kutaathiri maendeleo ya sekta zinazotegemea zaidi fedha za wahisani.
..