Alhamisi , 18th Feb , 2016

Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ndiyo yenye dhamana ya kusimamia huduma za afya kwa wananchi imesema itaendelea kutoa taarifa za mara kwa mara kwa wananchi kuhusu milipuko ya magonjwa ikiwamo kipindupindu.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu.

Taarifa hiyo iliyotolewa kwa vyombo vya habari imewataka viongozi wa mikoa na wilaya kuhakikisha upatikanaji wa taarifa sahihi, mapema kwa kuzingatia miongozo na kwa wakati bila kuficha pindi wanapopata wagonjwa wapya.

Pia taarifa hiyo imeeleza kuwa jamii isiwekewe vikwazo vya faini au kunyanyapaliwa wapatapo ugonjwa huo kwani inaweza kusababisha wananchi kuogopa kwenda katika vituo vya afya.

Aidha imewataka wakuu wa mikoa na wilaya wawasiliane na wizara iwapo kuna ufafanuzi wowote unaohitajika kwa taarifa zinazotolewa kuhusu magonjwa hayo ya mlipuko.