Jumatatu , 16th Jan , 2017

Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi Dkt. Charles Tizeba amelazimika kutoa ufafanuzi kuhusu hali ya chakula nchini huku akisisitiza kuwa Tanzania ina chakula cha kutosha na haina njaa kabisa.

Waziri wa Kilimo, Mifubo na Uvuvii, Dkt. Charles Tizeba

Dkt. Tizeba ametoa ufafanuzi huo leo wakati akiongea na waandishi wa habari, na kusema kuwa watu wanaoneza taarifa za kuwepo kwa njaa Tanzania wana lengo la kuingiza mahindi yao yasiyo na ubora ili wafanye biashara, jambo ambalo serikali imelikataa.

Akizungumzia uhalisia wa hali, amesema kilichotokea ni kupanda kwa bei ya mahindi, hali iliyosababishwa na uamuzi wa serikali kuuza nafaka hiyo katika mataifa jirani yaliyokuwa na uhitaji mkubwa, ingawa kiwango kilichouzwa kilikuwa ni sehemu ya mahindi ya ziada.

"Mwaka jana gunia la mahindi kwa bei ya wastani wa kitaifa ilikuwa 65,000 lakini sasa ni 85,000 na wala haijafikia mara mbili mara tatu kama inavyosemwa ingawa kuna maeneo kama rorya imefikia hadi 150,000 kutokana na wao kutegemea misimu miwili wakajikuta wanatumia akiba yao lakini hali ya hewa ikawa tofauti kwahiyo kuna wafanyabishara wakaamua kutumia hiyo fursa kupandisha bei zaidi" Amesema.

Ameendelea kusema ..... "Mavuno ya nafaka yalikuwa tani milioni 16 wakati mahitaji yakiwa tani milioni 13 kwahiyo ziada ilikuwa tani milioni 3, kwahiyo katika hiyo ziada milioni 1.5 ikasafirishwa nje, wenzetu walikuwa wananunua kwa gharama yoyote kwa kuwa walikuwa na shida, hiyo ndiyo maana bei ya nafaka imepanda sana hasa mahindi, kwa sasa bei imefika hadi mia 8 mia 9 na wauzaji ni walewale, kwahiyo hawezi kuuza ndani kwa bei ya chini lakini kupanda huko kulitarajiwa"

Amesema kupanda bei kwa mahindi kulitarajiwa na ni kwa kawaida na wala hakuwezi kumaanisha kuwa Tanzania kuna njaa wakati nafaka zote zinapatikana kila kona ya Tanzania

"Hakuna soko halina mahindi, hakuna soko halina mchele, hakuna soko halina maharage, masoko ya mijini yamejaa viazi..... nchi ina ziada tani milioni 3 kwanini mnataka tukanunue tena tani milioni 1 za nini?"

Kuhusu ukame, amesema ni kweli kuna hali ya upungufu wa mvua, na hiyo inafahamika maana ilishatabiriwa na kuwataka wananchi watunze akiba yao ya chakula na wasidanganyike kukiuza, kwa sababu hali ya hewa haitakuwa nzuri katika baadhi ya maeneo.

Tizeba ametaja Mikoa 11 kuwa na ukame baada ya kuwa na uhaba wa mvua na mtawanyiko usioridhisha na kupelekea mazao kunyauka.

Mikoa hiyo ni pamoja na Kagera, Mwanza, Geita, Kilimanjaro, Arusha, Mara, Pwani, Tanga, Morogoro, na sehemu ya Mkoa wa Shinyanga na Simiyu ambapo mimea iliyopandwa kwa baadhi ya maeneo imeathirika.

Amewasihi wananchi waache tamaduni ya kung'ang'ania chakula cha aina moja na kuwataka kutumia mchele na viazi kama wanaona mahindi yamepanda bei.. "Nafaka siyo mahindi tu, tunao mchele na mpunga wa kutosha, na viazi vipo kutoka Tunduma, watumie hivyo"

Waziri huyo amepiga marufuku mtu yoyote kutoa taarifa za njaa kwa kuwa serikali ndiyo inayojua hali ya chakula kupitia vyanzo vyake.