Jumanne , 5th Apr , 2016

Mamlaka ya Mapato nchini Tanzania TRA imevuka lengo la makusanyo kwa mwaka wa fedha unaoishia Juni mwaka huu ambapo katika kipindi cha miezi tisa iliyopita, mamlaka hiyo imekusanya jumla ya shilingi trilioni 9.88.

Kamishna Mkuu wa TRA Alphayo Kidata

Serikali imeiwekea Mamlaka ya Mapato TRA malengo ya kukusanya shilingi trilioni 12 hadi kufikia mwezi Juni mwaka huu.

Kamishna Mkuu wa TRA Alphayo Kidata amesema hayo leo wakati akitoa taarifa ya makusanyo kwa kipindi cha mwezi Machi mwaka huu ambapo makusanyo yamefikia shilingi trilioni 1.316 kati ya malengo ya kukusanya shilingi trilioni 1.3, kiasi ambacho ni sawa na asilimia 101.

Aidha, Bw. Kidata amesema mamlaka hiyo inakusudia kuongeza udhibiti wa vitendo vya ukwepaji kodi hususani biashara za magendo kwa kununua boti nne za mwendo kasi zitakazokuwa zikifanya doria ya saa ishirini na nne katika pwani ya bahari ya Hindi, eneo ambalo ni sugu kwa uingizaji wa magendo.