Ijumaa , 22nd Aug , 2014

Mamlaka ya Mawasiliano nchini (TCRA) imeanza zoezi la kuzunguka nchi nzima kwa ajili ya kutoa mafunzo kwa jeshi la polisi kwa lengo la kupambana na uhalifu unaofanyika kupitia mitandao ya mawasiliano.

Meneja Mawasiliano wa Mamlaka ya Mawasiliano nchini Tanzania (TCRA) Bw. Innocent Mungi.

Meneja Mawasiliano wa (TCRA) Innocent Mungi amesema leo kuwa polisi wakiwa walinzia wa amani na usalama wa raia wanapaswa kujipanga katika kufanya kazi yao vizuri kwa kushirikiana na mamlaka hiyo ili kudhibiti uhalifu unaofanyika kwenye mitandao.

Amesema watu wanafikiri jukumu la kukamata watu wanaotumia mawasiliano vibaya ni la TCRA bila kujua kwamba ni la polisi huku TCRA wakiwa na jukumu la kutoa ushirikiano tu kwa jeshi hilo ili kufanikisha kuwapata wahalifu hao.

Wakati huo huo, wananchi wa vijiji 120 vilivyopo mkoa wa Arusha wanatarajia kuanza kunufaika na huduma ya umeme kupitia mpango wa kusambaza umeme vijijini unaofadhiliwa na (REA) na kutekelezwa na shirika la umeme la taifa (TANESCO).

Afisa Uhusiano na Huduma kwa wateja ,wa shirika la umeme Arusha, Benedict Nkini amesema kuwa kwa sasa wako katika hatua ya kutoa elimu kwa wananchi juu ya mradi huo ili waweze kujiandaa kuunganishwa na huduma hiyo.

Kwa upande wake Afisa Masoko wa Tanesco,Adelina Lyakurwa amesema kuwa amewaomba wananchi kutumia fursa hiyo kuunganishiwa umeme huo wa bei nafuu ambao Mtanzania wa hali ya chini anaweza kuumudu.