Alhamisi , 14th Mar , 2024

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema Serikali imedhamiria kuhakikisha usalama wa nchi na mipaka yake dhidi ya majanga mbalimbali unaendelea kuimarishwa ili kujiandaa na kuwa na utayari wa kukabiliana na majanga, maafa na dharura yoyote.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akitoa neno wakati wa ufungaji wa mafuzo ya zoezi la utayari dhidi ya dharura za kikemikali na kimionzi Tanzania, katika viwanja vya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Bandarini jijini Dar es Salaam.

Ametoa kauli hiyo leo Alhamisi, Machi 14, 2024 wakati wa ufungaji wa mafuzo ya zoezi  la utayari dhidi ya dharura za kikemikali na kimionzi Tanzania, katika viwanja vya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Bandarini jijini Dar es Salaam.
 
Amesema kuwa moja ya jitihada hizo ni pamoja na kukamilisha maandalizi ya nyaraka mbili muhimu za Mpango wa Kitaifa wa Maafa ya Kikemikali, Kibaiolojia, Kiradiolojia na Kinyukilia. (CBRN National Action Plan) na Mpango wa Kuitikia wakati wa Dharura za Kinyuklia na Kiradiolojia (Radiological and Nuclear Response Plan) ambazo alizizindua katika hafla hiyo.
 
“Kupitia nyaraka hizi, mmeweka mikakati ya pamoja ya kitaifa ya namna ya kukabiliana na kujikinga na majanga yatokanayo dharura za kikemikali, kibaiolojia, kiradiolojia na kinyuklia. Nimefurahi sana kusikia nyaraka hizo zimezingatia masuala muhimu ya kisera, uzoefu wa kukabiliana na majanga kitaifa na kimataifa pamoja na matakwa ya kisheria na itifaki za kimataifa.”
 
Aidha, Mheshimiwa Majaliwa amezitaka wizara zote na taasisi zinazohusika na kutekeleza mipango hiyo kuitumia kikamilifu na zitoe ushirikiano kwa wote wanaohitaji kutekeleza miongozo hiyo “Miongozo hii isiwe ni nyaraka za makabatini tu bali iwe miongozo ya utekelezaji wa hatua thabiti za kuhakikisha tunajenga nchi imara na salama. ”
 
Kwa upande wake, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda amesema mafuzo ya zoezi  la utayari dhidi ya dharura za kikemikali na kimionzi yalilenga kuwapa washiriki maarifa na ujuzi wa kukabiliana na vitisho vya kikemikali, kiradiolojia, kinyuklia na kusaidia juhudi kujiandaa na kukabiliana na majanga hayo katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
 
Ameongeza kuwa nyaraka zilizozinduliwa na Mhe. Majaliwa zitatumika kuwa nyaraka za kitaifa na miongozo inayochukua mitizamo na mahitaji ya taasisi na wizara mbalimbali za Serikali na wadau wengine waliopewa majukumu katika nyanda za kemikali, kibaolojia, kiradiolojia na nyuklia

“Lengo kuu la mipango hii ni kuweka mikakati ya pamoja kama Taifa ya namna ya kukabiliana na kujikinga na majanga hayo.”
 
Kwa Upande wake, Mkemia Mkuu wa Serikali Dkt. Fidelice Mafumiko amesema kuwa  mazoezi ya utayari dhidi ya dharura za kikemikali na kimionzi yataendelea kufanyika mara kwa mara kwa lengo la kujenga utayari wa timu ya Taifa ya kujiandaa kukabiliana na dharura za kitaifa.