Jumanne , 14th Jun , 2016

Taasisi za kifedha nchini zimeshuriwa kutumia sehemu ya faida wanayopata kwa kuboresha upatikanaji wa huduma za kijamii kama vile afya, elimu maji na barabara ili kuboresha maisha ya wananchi ambao ndiyo wateja wa baadaye wa taasisi hizo.

Mkuu wa Utumishi wa Benki ya Eximu Bw. Frederick Kanga

Mkuu wa Utumishi wa Benki ya Eximu Bw. Frederick Kanga, ametoa wito huo wakati wateja na wafanyakazi wa benki hiyo waliposhiriki zoezi la uchangiaji damu kwa Mpango wa Taifa wa Damu Salama, zoezi linalotekelezwa chini ya miradi ya maendeleo kwa jamii ambapo kwa mwaka huu wa fedha zaidi ya shilingi bilioni 1.9 zimetengwa kwa ajili ya miradi hiyo.

“Mbali ya kufanya biashara sisi kama benki tumeona ni bora tushiriki katika miradi inayolenga kuboresha maisha ya Watanzania ambao tunadhani baadaye ndiyo watakuwa wateja wetu...kwa kuchangia damu tuna imani kwamba tutakuwa tumeokoa maisha ya idadi kubwa ya Watanzania wenye mahitaji ya damu,” amesema Bw. Kanga.

Kwa upande wake, Afisa Ushawishi kutoka Mpango wa Taifa wa Damu Salama Fatma Mjungu amezungumzia umuhimu wa watu kuchangia damu na namna vijana wanavyotakiwa kulinda afya zao dhidi ya magonjwa yanayoambukizwa kwa njia ya damu.

“Jambo la msingi ninaloliomba kwa taasisi mbali mbali za kifedha nchini ni kuiga mfano huu wa benki ya Exim kwa kushiriki kujitolea damu huku vijana wakijenga utamaduni wa kuishi maisha yatakayowaepusha dhidi ya magonjwa yanaoambukizwa kwa njia ya damu ili hata damu wanayochangia iwe safi na kutumika,” amesema Bi. Fatma.