Jumanne , 20th Oct , 2015

Kuelekea uchaguzi mkuu utakaofanyika Octoba 25 mwaka huu Serikali imetakiwa kukabiliana na viashiria vya uvunjifu wa amani na kuvipatia ufumbuzi ili kuhakikisha uchaguzi huru na wa haki utakaodumisha amani ya taifa.

Mwenyekiti wa Kamati ya Amani ya Apet Jijini Arusha Peter Aham

Hayo yameelezwa na mwenyekiti wa kamati ya amani ya Apet Jijini Arusha Peter Aham katika mjadala wa masuala ya amani hasa katika kipindi cha uchaguzi ulioudhuriwa na wawakilishi kutoka tume ya uchaguzi, Jeshi la polisi, vyama vya siasa pamoja na wadau wa amani.

Peter Ahham amesema kumekuwa na dalili za wazi za baadhi ya mamlaka kuonekana kuegemea upande mmoja ikiwemo tume ya uchaguzi, jeshi la polisi na baadhi ya vyombo vya habari jambo ambalo linapingana na taaluma na weledi na linaweza kuathiri amani

Mkuu wa wilaya ya Arusha Fadhili Nkulu amesema kuwa kwa muda mrefu amani iliyodumu nchini imekuwa ikihatarishwa na masuala ya udini, ukabila na itikadi za kisiasa hivyo kila mtanzania ana jukumu la kulinda amani katika kipindi hiki cha uchaguzi.

Kwa upande wake mkurugenzi wa shirika lisilokuwa la kiserikali la USIP ,Dr. James Jesse pamoja na kamishna wa polisi mkoa wa Arusha Edward Balele amesema kuwa kila mtanzania, vyama vya siasa vina wajibu wa kulinda amani na kuhakikisha kuwa uchaguzi unakuwa huru na salama.