Jumanne , 26th Aug , 2014

Tume ya haki za binadamu na utawala Bora nchini Tanzania imeitaka serikali kufanya uchunguzi wa kina kubaini wanaochochea, kufadhili na kutekeleza vitendo vya mauaji na ukatili dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi (Albino).

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto nchini Tanzania Bi. Sophia Simba.

Taarifa iliyotolewa na Kamishna wa tume hiyo Mh Ally Hassan Rajabu imeongeza kuwa Serikali kupitia wadau mbalimbali inatakiwa kuongeza kasi ya utoaji wa elimu ya haki za binadamu na maadili kwa jamii ili kukomesha ukatili huo nchini Tanzania

Aidha tume hiyo pia imetoa wito kwa jamii kushirikiana na vyombo vya dola kutoa taarifa juu wa watu wenye mienendo yenye kutiliwa shaka wakiwemo wanafamilia za watu wenye ulemavu wa ngozi ambao uchunguzi wa tume umebaini kwamba baadhi ya watu wa karibu na familia wamekuwa wakitumika kusaidia kufanikisha vitendo vya ukatili dhidi yao.

Wakati huo huo, Serikali imesema ushiriki hafifu wa wananchi katika kutoa taarifa za watoto wanaolewa nchini umekuwa ukichangia kwa kiasi kikubwa kuongezeka kwa ndoa za utotoni hali inayopelekea watoto hao kukosa fursa ya kupata elimu.

Akiongea jana Jijini Dar es Salaam Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto Bi. Anna Tayari Maembe amesema baadhi ya jamii zilizopo katika kanda ya ziwa zimekuwa zikishiriki kuoza watoto wao na hivyo kuwahatarishia maisha yao huku sheria ya ndoa nayo ikiwa ni kikwazo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha waandishi wa Habari Wanawake nchini TAMWA, Bi. Valerie Msoka amesema usiri mkubwa uliopo miongoni mwa wazazi na walezi unaochangiwa na umasikini katika familia hizo umesababisha watoto wengi kuolewa wakiwa na umri mdogo.