Jumatatu , 22nd Sep , 2014

Serikali ya Tanzania imeidhinisha zaidi ya shilingi bilioni 290, kwa ajili ya kuboresha daftari la kudumu la wapiga kura ili liwe la kidijitali, zoezi litakaloendeshwa na kusimamiwa na tume ya taifa ya uchaguzi - NEC.

Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi nchini Tanzania NEC, Jaji Mstaafu Damian Lubuva.

Mwenyekiti wa NEC Jaji Mstaafu Damian Lubuva, amesema hayo leo jijini Dar es Salaam na kufafanua kuwa kutolewa kwa fedha hizo kutaiwezesha tume hiyo kuanza mara moja uboreshaji wa daftari hilo, zoezi lililochelewa kwa zaidi ya mwezi mmoja kutokana na kutokwepo kwa fedha.

Kuidhinishwa kwa fedha hizo kumekuja licha ya wadau viiwemo vyama vya siasa, kuhoji wapi tume ya uchaguzi itazipata fedha hizo, kutokana na bajeti iliyotengwa na bunge kwa ajili ya utendaji wa ofisi hiyo kuwa ni zaidi ya mara kumi ya kiwango kilichopangwa kutumika kwenye uboreshaji daftari la wapiga kura.

Mmoja wa wadau waliolalamikia fedha hizo ni Mwenyekiti wa Chama cha upinzani cha CUF Profesa Ibrahim Lipumba ambaye amesema inashangaza kuona serikali inapanga matumizi ya fedha ambayo hayajaidhinishwa na bunge.

Aidha, Profesa Lipumba ameongeza kuwa hata teknolojia itakayotumiwa kwenye daftari hilo ina mapungufu mengi kwani tofauti na inavyoelezwa kuwa itafanya uhakiki na utambuzi wa wapiga kura kuwa rahisi, teknolojia hiyo imeonyesha mapungufu makubwa kwenye nchi ilikotumika ikiwemo nchi za Kenya na Malawi.