Jumatano , 2nd Dec , 2015

Jeshi la Polisi jijini Dar es Salaam likishirikiana na maafisa wa Forodha na Mamlaka ya Kodi ya Mapato Tanzania (TRA) limeyakamata makontena tisa maeneo ya Mbezi Beach Tank Bovu yakiwa yameshushwa katika eneo ambalo siyo rasmi kuhifadhi makontena.

Mkurugenzi wa Elimu kwa walipa Kodi wa Mamlaka ya Kodi Tanzania TRA Richard Kayombo.

Mkurugenzi wa elimu kwa mlipa Kodi wa Mamlaka ya Kodi Tanzania TRA Richard Kayombo amesema kulingana na nyaraka za makontena hayo yalikuwa yanatakiwa kupelekwa bandari kavu ya EPZ iliyoko Ubungo jijini Dar es Salaam lakini yakapelekwa Mbezi Beach.

Kayombo amewataka wamiliki na wakala wa forodha aliyehusika na utoaji wa makontena hayo katika bandari ya Dar es alaam kujitokeza ndani ya masaa 24 vinginevyo TRA itayafungua makasha na kutambua kuna kitu ngani na kama yatakuwa bidhaa halali zitataifishwa na kama ni bidhaa haramu zitateketezwa kwa mujibu wa sheria.

Kayombo amesema lengo la kukamata makontena hayo ni kujiridhisha uhalali wa makontena hayo ambayo yalitolewa usiku wa manane kuamkia jana bandari ya Dar es Salaam zikiwa na maelekezo ya kuelekea bandari ya nchi kavu ya vingunguti.

Kayombo amesema bado kuna sintofahamu ya makontena hayo kutokana na kukamatiwa maeneo ya Tang bovu badala ya Vingunguti yalipokuwa yanapaswa kupelekwa.