Jumamosi , 2nd Mei , 2015

Mamlaka ya mapato TRA mkoani Iringa kupitia idara ya huduma na elimu kwa mlipakodi imewataka wamiliki wa pikipiki na bajaji kutumia kikamilifu muda ulioongezwa kusajili pikipiki zao.

Meneja wa Mamlaka ya Mapato Mkoa wa Iringa Rosalia Mwenda akitoa taarifa kwa vyombo vya habari ofisini kwake.

Afisa elimu wa idara ya huduma na elimu kwa mlipa kodi mkoani iringa Bw. Faustina Masunga amesema kuwa pamoja na serikali kuongeza muda wa wamilki hao wa pikipiki na bajaji kufanya usajili wa vyombo vyao bado wamekuwa wakisuasua katika kutekeleza zoezi hilo.

Bw. Masunga ameyasema hayo kufuatia malalamiko ya hivi karibuni ya waendesha pikipiki kulalamikia shughuli za usajili kukumbwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutumia muda mrefu.

Aidha, ameongeza kuwa baadhi ya wamiliki wamekuwa wakilalamikia gharama za kusajili vyombo hivyo vya moto kutofautiana na kupelekea kudhani kuwa kuna utapeli ilihali ni gharama za kawaida kutokana na malimbikizo ya madeni ya wamiliki hao.

Pia, amebainisha kuwa kuna watengezaji wa vibao vya pikipiki na bajaji ambao wamesajiliwa kwajili ya kazi hiyo na hivyo kurahisisha utoaji wa huduma hiyo kwa wahitaji.

Hata hivyo, afisa elimu wa idara ya elimu na huduma kwa mlipa kodi wa TRA mkoani Iringa Bw. Faustine Masuga ametoa wito kwa wamiliki wa pikipiki ambao wapo nje ya manispaa kwenda katika vituo vya polisi kwaajili ya ukaguzi na kuja na fomu ya ukaguzi kwaajili ya kulipia na kuchukua kadi.