Jumamosi , 17th Oct , 2020

Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Hamisi Kigwangalla amesema katika wizara hiyo wameanzisha mkakati maalum wa kumuenzi Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na tayari wameunda kamati maalum ambayo itashughulika na suala hilo.

Nyumba ya Hayati Baba wa Taifa Mwl. Julius Nyerere, iliyoko maeneo ya Magomeni

Dkt Kigwangalla amesema hayo leo jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa nyumba kumbukizi ya Mwalimu Julius Kambarege Nyerere aliyowahi kuishi wakati wa harakati za kudai uhuru iliyopo Magomeni jijini Dar es salaam 

“Tayari nimeshaunda kamati itakayosimamia kuhakikisha yale mambo ambayo Baba wa Taifa ameyafanya yanaenziwa, sambamba na kuviweka vitu vyote alivyotumia kama kumbukumbu muhimu kwa taifa.’’amesema Dkt.Kigwangalla. 

Kwa upande wake Waziri Mkuu Mstaafu Jaji Joseph Sinde Warioba amesema Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere bado hajaenziwa ipasavyo, hivyo kumtaka Waziri Kigwangalla kushirikiana na Mkurugenzi wa Makumbusho ya Taifa kufanya maboresho yote ya maeneo ambayo Baba wa Taifa alikua akifanya kazi.

“Bado kuna maeneo mengine ambayo Baba wa Taifa ameyatumia wakati wa harakati za kudai uhuru,hiyvo yanapaswa kutambulika kihistoria’’, amesema Jaji Warioba

Naye mtoto wa Hayati Baba wa Taifa ,Mwalimu Nyerere,Makongoro Nyerere, akiwa mmoja wa waliohudhuria uzinduzi wa nyumba kumbukizi, amefurahishwa na jinsi serikali inavyomuenzi baba yao na kuwasihi Watanzania kujifunza historia aliyoiacha Baba wa Taifa na si kusubiri siku maalum

Nyumba hiyo imezinduliwa leo baada ya ukarabati, ilitumiwa na Baba wa Taifa wakati wa harakati za kudai uhuru na ndani yake vimehifadhiwa vitu mbalimbali alivyotumia Mwalimu ikiwemo cherehani iliyotumika kuzishona nguo zake.