Ijumaa , 26th Feb , 2016

Mamlaka ya mapato nchini Tanzania(TRA), kupitia dalali wake Yono Action Mart imekusanya shilingi milioni 200 kutoka kwa kampuni sita zinazodaiwa kukwepa kodi baada ya kutorosha makontena kwenye bandari kavu (ICD) ya Azam.

Mabaunsa wa kampuni ya udalali ya Yono Auction Mart wakiwa wameimarisha ulinzi

Akizungumza na waandishi wa habari jana Jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa bodi ya kampuni ya Yono, Stanley Kivela amesema kampuni 24 ziliisababisha serikali hasara ya shilingi bilioni 18 kwa kutorosha makontena bila kulipia Ushuru.

Bw. Yono amesema fedha hizo ni za kampuni sita ambazo zimeitikia agizo la serikali baada ya notisi waliyopewa kuisha jana huku akiongeza kuwa fedha hizo ni pamoja na faini ya ulipaji kodi hiyo.

Aidha ameongeza kuwa kampuni hiyo iliyopewa kazi ya kuwafuatilia wadaiwa hadi jana wamekusanya shilingi milioni 200 pia wamekamata mali za kampuni mbili ambazo ni kontena tisa za bati pamoja na maghorofa.

Pia mwenyekiti huyo amesema zoezi hilo linaendelea kwa kuwa wamefanya kwa kampuni sita tu kati ya 24 wanazozifuatilia na kusema kampuni 18 wataanza zoezi la kukamata mali zao kwa ajili ya kuweza kulipa kodi hiyo waliyoikwepa.