Jumatatu , 7th Dec , 2015

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe Magufuli amevunja bodi ya Mamlaka ya Bandari nchini (TPA) pamoja na kutengua uteuzi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Dk. Shaaban Mwinjaka

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza na waandishi wa habari hawapo pichani

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe Magufuli amevunja bodi ya Mamlaka ya Bandari nchini (TPA) pamoja na kutengua uteuzi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Dk. Shaaban Mwinjaka, Mwenyekiti wa Bodi ya Bandari Profesa Joseph Msambichaka pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Bandari, Awadh Massawe.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jijini Dar es Salaam leo, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema kutenguliwa kwa uteuzi huo kunatokana na ziara alizofanya katika bandari ya Dar es salaam na kubaini uwepo wa mianya ya ukwepaji kodi ikiwemo ya makontena 2,387 yaliyopitishwa kati ya Machi na Septemba mwaka jana.

Amesema upotevu huo unatokana na mfumo usiokidhi wa kupokelea malipo ambao unatoa mwanya wa kupoteza mapato ya serikali na kutaka mfumo huo ubadilishwe kufikia Desemba 11.

Waziri Mkuu, Majaliwa amesema kuwa kutokana na utendaji huo mbovu wa bandari, ripoti iliwataja waliohusika na upitishaji wa makontena hayo na bila ya kuwepo kwa taarifa yoyote, hivyo amewasimamisha kazi wasimamizi 8 wa bandari kavu (ICD) ambao ni Happygod Naftari, Juma Zaar, Steven Naftari Mtui, Titi Ligalwike, Lydia Prosper Kimaro, Mkango Alli, John Elisante pamoja na James Kamwomwa.

Wengine ambao hawakuwemo kwenye ripoti hiyo ambao ni viongozi wa sekta zilizotoa ruhusa makontena kutoka ndani ya bandari lakini ni wahusika wakuu ambao ni Shaban Mngazija aliyekuwa meneja mapato, Rajab Mdoe mkurugenzi wa fedha na mkuu wa bandari kavu, Ibin Masoud kaimu mkurugenzi wa fedha, Apolonia Mosha meneja wa bandari msaidizi (Fedha).

Waziri Mkuu, amesema kuwa katika ziara yake kwa shirika la reli nchini (TRL) alibaini matumizi mabaya ya fedha ya Sh. Bilioni 13 nje ya utaratibu ambao uchunguzi unakamilishwa kwa waliohusika.