Jumanne , 29th Mar , 2016

Wauguzi na Madaktari wa hospitali ya Mkoa wa Mtwara (Ligula),wamegoma kutoa huduma hii leo kwa madai ya kutaka serikali iweze kuchukua hatua za haraka juu ya waliohusika na tukio la kupigwa na kudhalilishwa kwa daktari mmoja hospitalini hapo.

Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mkoa wa Mtwara, Ligula, Dkt. Shaibu Maarifa

Wakiongea na mwandishi wetu hospitalini hapo watumishi hao wa hospitali hiyo wamesema kuwa licha ya kutaka tukio hilo lichukuliwe hatua lakini wanataka walipwe stahiki zao nyingine na kurekebishiwa maslahi yao ili waweze kurejea kazini.

Wakiongea na East Africa Radio, baadhi ya wagonjwa wagonjwa waliokwenda kupata matibabu katika hospitali hiyo wamesema tangu asubuhi mpaka kufikia sasa hakuna huduma yoyote waliyoipata hali inayohatari hali zao za kiafya huku wakiwa hawajui hatma yao.

Wakati taarifa hii inatufikia Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu amewasili katika hospitali hiyo ya Ligula kwa ajili ya Ukaguzi huku akitarajiwa kutoa kauli juu ya tukio hilo.

Hivi karibuni ilidaiwa Daktari Mmoja wa Hospitali ya Ligula alifahamika kwa jina la Dkt. Dickson Sahini, alipigwa na wananchi na kisa kudhalilshwa kwa kuvuliwa nguo kitendo ambacho kimewafanya madaktari hao kugoma.