Ijumaa , 5th Dec , 2014

Mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali, Profesa Mussa Juma Asad amesema kuwa kuchanganya siasa na biashara na matatizo ya watu binafsi, katika shughuli za kiutendaji za ofisi yake ni kufanya kosa.

Rais Jakaya Mrisho kikwete akimuapisha Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG) Profesa Musa Juma Assad.

Asad amesema hayo jana mbele ya waandishi wa habari mara baada ya kufunguliwa kwa mkutano mkuu wa kila mwaka wa wahasibu na wakaguzi {NBAA} uliofanyika jijini Arusha katika jengo la AICC.

Amesema ofisi ya CAG na watendaji wengine watafanya kazi kwa kufuata maadili ya kazi na aliwaasa wana siasa na wafanyabishara kila mmoja aheshimu taaluma yake kwa faida ya nchi.

Mdhibiti Mkuu huyo ameendelea kusema kuwa iwapo kila mmoja atawajibika katika nafasi yake na kuaminiana katika shughuli za kila siku, ziwe na kitendaji na biashara hakutakuwa na matatizo yoyote.

Asad amesema kila mtaalamu wa fani hiyo anapaswa kujifunza mambo mapya, kwani kila kukicha teknolojia inakua hivyo nao wanapaswa kwenda na wakati.

Awali akifungua mkutano huo, Naibu Waziri wa Fedha Adamu Malima amewataka wataalamu wa uhasibu na ukaguzi kuwa wazalendo wa kweli kwa kulinda rasilimali za nchi ikiwa ni pamoja na kufuata maadili ya kazi yao bila ya kuyumbishwa.

Waziri Malima amesema iwapo hilo litazingatiwa ana uhakika mkubwa wa uchumi wa nchi kukua kwani taaluma hiyo ni kiini cha matatizo yote ya ulaji fedha hivyo wanapaswa kuwajibika kikamilifu.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya NBAA, Isaya Jairo amesema na kuwataka wataalamu kufanya kazi katika viwango vya kimataifa kwa masilahi ya nchi.

Jairo amesema kuwa kwa sasa bodi hiyo itawaleta wataalamu kutoka nje, kwa ajili ya mafunzo ya kazi katika sekta ya gesi na madini ili waweze kufanya shughuli hiyo kwa weledi mkubwa.