Alhamisi , 15th Jan , 2015

Watanzania wametakiwa kuisoma na kuielewa vyema Katiba Inayopendekezwa na Bunge Maalumu la Katiba na muda ukifika kuipigia kura ya ndiyo kwani imebeba mambo mengi yenye manufaa kwa wananchi wa pande zote mbili za muungano.

Katibu mkuu wa Chama Cha Mapinduzi CCM Abdulrahman Kinana

Katibu mkuu wa Chama Cha Mapinduzi CCM Abdulrahman Kinana ametoa rai hiyo kwenye wilaya ya mjini, wakati wa siku ya kwanza ya ziara yake ya siku kumi kwenye visiwa vya Unguja na Pemba ambapo, amewaomba wananchi kuisoma kwa makini na kuilewa Katiba Inayopendekezwa kwani ina mambo mengi mazuri hususani yahusuyo muungano.

Nao baadhi ya wananchi wa Unguja wamesema kuwa wanachotaka wananchi ni kuona panakuwepo na amani na utulivu ili kuwaruhusu kufanya shughuli za kujiletea maendeleo na kuitaka serikali kuwasikiliza wananchi kile wanachokihitaji na wakitekeleze.

Akiwa katika wilaya ya mjini katibu huyo wa CCM taifa Abdulahaman Kinana, alishiriki shughuli mbalimbali za maendeleo na kuzindua miradi ya maji ikiwemo mradi wa maji wa skuli ya Makadara Msingi, iliyopo shehia ya Makadara kabla ya kuelekea kwenye mradi mkubwa wa vikokotoni na kushiriki ujenzi wa ofisi za chama na kukabidhi vifaa vya michezo kwa timu za mpira wa miguu.