Jumanne , 28th Apr , 2015

Mbunge wa Mpanda Mjini kupitia tiketi ya Chama cha Demkrasia na Maendeleo CHADEMA amesema kuwa hakubaliani na katiba ya chama chake hususani kifungu kinachomzuia mwanachama kwenda mahakamani endapo ataona hajatendewa haki ndani ya chama chake.

Mbunge wa Mpanda Mjini Said Arfi

Mbunge wa Mpanda Mjini kupitia tiketi ya Chama cha Demkrasia na Maendeleo CHADEMA amesema kuwa hakubaliani na katiba ya chama chake hususani kifungu kinachomzuia mwanachama kwenda mahakamani endapo ataona hajatendewa haki ndani ya chama chake.

Arfi ameyasema hayo leo akiwa katika kipindi cha HOT MIX cha EATV, na kusema kuwa kifungu hicho kilicho ndani ya Katiba ya chama hicho kinapingana na Katiba ya nchi.

“Katiba ya CHADEMA naikubali kama katiba ya chama changu, lakini kifungu hicho sikubaliani nacho” aamesema Arfi.

Mbunge huyo pia amesema kuwa hakubaliani na maamuzi ya chama hicho ya kumfukuza uanachama aliyekuwa mbunge wa Kigoma Kaskazini Zitto Kabwe kwa kukiuka kifungu hicho tena bila kufuata utaratibu za vikao.

“Hata kama Zitto alikosea, ilikuwa ni lazima vikao halali vya chama vikae ndiyo viamue, siyo kwa utaratibu uliotumika”

Akizungumzia msimamo wake ndani ya chama hicho, Arfi amesema kuwa yeye bado ni mwanachama hai wa CHADEMA kwa kuwa bado chama hicho hakijamfukuza, na kukiri kuwa aliingia katika mgogoro na viongozi wenzake wakati akiwa Makamu Mwenyekiti wa chama hicho kutokana na kutokubaliana na mwenendo wa baadhi ya viongozi wakuu wa chama hicho.

“Ni kweli tulikuwa na mgogoro uliotokana na mimi kutokubaliana na mwenendo wa viongozi na nikaamua kujiuzulu nafasi yangu, kwa sasa hatuna tatizo tena”

Kuhusu uwezekano wa chama hicho kumfukuza, Arfi amesema kuwa hana tatizo endapo atafukuzwa uanachama, na kwamba hawezi kusubiri kufukuzwa ndani ya chama hicho, isipokuwa “nitatafakari kabla ya kumalizika kwa mkutano wa Bunge na nitafanya maamuzi kama ninatosha kuendelea kuwa CHADEMA, maamuzi yangu nitayatangaza kabla Bunge halijakwisha”

Arfi ametetea uamuzi wake wa kuendelea kubaki ndani ya Bunge Maalum la Katiba na kusema kuwa alikwenda bungeni kuliwakilisha taifa na siyo chama. “Sikwenda katika bunge lile kuiwakilisha CHADEMA”

Amesema msimamo wake ni kuipinga Katiba Inayopendekezwa, kwa kuwa haijajengwa katika misingi ya muundo wa muungano wa serikali tatu.

Kuhusu Uchaguzi ujao, Arfi amesema kuwa bado hajaamua kugombea, lakini kama CHADEMA wakiamua kumfukuza, atawaachia wananchi wa Mpanda wampe muongozo juu ya nini cha kufanya na ni chama gani ataenda kugombea.

Nje ya studio, Arfi amesema kuwa kuna uwezekano mkubwa wa yeye kustaafu siasa.