Alhamisi , 4th Feb , 2021

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli, amemshauri mwanamke aliyedai kuwa mume wake alikuwa ni askari magereza na alifukuzwa kazi baada ya kusingiziwa kwamba aliwapelekea wafungwa simu, watafute kazi nyingine si lazima mume wake awe askari magereza.

Dkt. John Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Kauli hiyo ameitoa hii leo Februari 4, 2021, mara baada ya kuzindua nyumba 24 za maaskari wa Gereza Kuu Isanga jijini Dodoma, na ndipo akina mama walijitokeza wakimuomba asikilize shida zao na awasaidie

"Magereza yetu tunatakiwa tujenge nidhamu sasa akifukuzwa si ukatafute shughuli nyingine huyo mume wako kwani lazima aliambiwa atakaa tu kwenye magereza na yeye amesingiziwa kosa la kupeleka simu nne kwa wafungwa", amesema Rais Dkt. Magufuli.

Awali Rais Dkt. Magufuli, alimshauri mwanamke huyo kuonana na Mkuu wa Magereza, "Wewe mama mume wako alifukuzwa, mambo ya Jeshi yana sheria zake, muone Mkuu wa Magereza lakini mimi nitajua ukweli uko wapi wakati nafahamu kweli kuna Maaskari Magereza siyo waaminifu wanawapelekea simu wafungwa na wengine hadi gongo na bangi".