Jumatano , 7th Apr , 2021

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Simon Sirro amewaagiza Makamanda wa Polisi wa mikoa ya Mtwara, Lindi, Dar es Salaam, Tanga, Pemba pamoja na Unguja kisiwani Zanzibar kufanya operesheni ya pamoja kudhibiti makosa ya dawa za kulevya.

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Simon Sirro

IGP Sirro ametoa maagizo hayo leo akiwa kisiwani Zanzibar ambapo amesema katika kipindi cha miezi mitatu makosa ya jinai yamepungua kwa asilimia 19.1 huku ya usalama barabarani yakipungua kwa asilimia 14.

"Bado madawa ya kulevya ni shida lakini makamanda wa mkoa wa Mtwara, Lindi, Tanga, Dar es Salaam na makamanda wote wa Pemba na wa Unguja ni lazima wafanye operesheni za pamoja hili suala haliwezi kutushinda uwezo mkubwa tunao kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama tuwashughulikie sana sana," amesema IGP Sirro.

Pia IGP Sirro amemdelea kusisitiza kwa viongozi wa dini kushirikiana na polisi ili kukabiliana na suala mtambuka la matukio ya udhalilishaji wa kijinsia.

"Bado makosa ya uzalilishaji ni suala ambalo ni mtambuka,  jeshi la polisi pekee yake hawawezi wakalimaliza hili tatizo nasisitiza tena viongozi wa dini watusaidie, sheria ni msumeno wewe Sheikh ukifanya kosa sheria ichukue mkondo wake, na Padri akifanya kosa sheria ichukue mkondo wake lakini ni elimu ni msingi sana watu wabadilishe fikra zao," amesema IGP Sirro.