Alhamisi , 28th Mar , 2024

Katika kipindi cha mwaka 2022/2023 deni la taifa limeongezeka kwa asilimia 15% na kufikia Trilioni 82.25 kutoka mwaka 2021/2022 huku deni hilo likitajwa bado kuwa ni himilivu.

Rais DK.Samia Suluhu Hassan akipokea Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Bw. Charles Kichere kwa mwaka 2022/23 Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 28 Machi, 2024.

Hayo yamebainishwa na Mkaguzi Mkuu wa hesabu za serikali nchini Charles Kichere wakati uwasilishwaji wa Ripoti ya CAG na ripoti ya TAKUKURU kwa mwaka 2022/2023 kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Samia Suluhu Hassan Ikulu ya Chamwino Dodoma.

“Hadi kufikia tarehe 30 Juni 2023 deni la serikali lilikuwa Trilioni 82.25 sawa na ongezeko la asilimia 15 kutoka mwaka 2021/2022 na deni hili bado ni himilivu” - CAG Charles Kichere

Aidha katika ripoti hiyo uchunguzi umeonesha kuwa baadhi ya mashirika ya Umma yamepata hasara zaidi ukilinganisha na ripoti iliyopita ya mwaka 2021/2022.

“Shirika la ndege Tanzania (ATCL), limepata hasara ya Shilingi Bilioni 56.64 ni sawa ongezeko la 61% kutoka hasara ya shilingi bilioni 35.24 kwa mwaka uliopita. “ - CAG, Charles Kichere

Kwa upande wake CP. Salum R. Hamduni Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU  amebainisha kuwa  Katika ufuatiliaji waliofanya wamebaini kuwa kati ya miradi 1800, miradi 171 yenye thamani ya shilingi Bilioni 143.3 ilikuwa na utekelezaji hafifu.

“Katika ufuatiliaji wa miradi 1800, miradi 171 yenye thamani ya shilingi Bilioni 143.3 ilibainika kuwa na utekelezaji hafifu na tulianzisha uchunguzi miradi hiyo.” Amesema CP Hamduni.

 Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ameahidi kuwa dosari zote zilizobainishwa kwenye ripoti zilizopokelewa leo zitafanyiwa kazi.