Jumatatu , 25th Mei , 2015

Zoezi la uandikishaji wapiga kura kwa kutumia mfumo mpya wa kielektoronik BVR umelalamikiwa na wananchi katika manispaa ya Kigoma Ujiji kutokana na kuchelewa kuandikishwa licha ya wananchi kulala kwa zaidi ya siku mbili katika vituo vya kuandikishia.

Zoezi la uandikishaji wapiga kura kwa kutumia mfumo huo limeanza katika kata za Kagera, Buhanda, Businde, Machinjioni, Rubuga na Kasimbu huku kata nyingine zikisubiri awamu ya pili hali ambayo inawafanya wananchi wa kata nyingine kwenda kujiandikisha katika kata zilizoanza zoezi hilo kutokana na ukosefu wa taarifa sahihi.

Kutokana na hali hiyo wameomba kuongezwa kwa muda wa uandikishwaji wapiga kura na kuweka utaratibu mzuri ambao utawezesha wananchi wote wenye sifa kuandikishwaji.

Kwa upande wake afisa mwandikishaji msaidizi katika kata ya Buhanda Sufiani Baruani amesema zoezi hilo linakabiliwa na tatizo la idadi kubwa ya wananchi kulingana na uwezo wa mashine zilizopo.

Awamu ya kwanza ya uandikishaji wapiga kura mkoani Kigoma imeanza katika baadhi ya kata Mei 21 huku ikiripotiwa kusimama kwa zoezi hilo katika kata ya Nguruka kutokana na kuishiwa kadi huku maelfu ya wananchi wakiwa bado hawajaandikishwa.

Tags: