Ijumaa , 15th Jan , 2016

Asasi za kijamii na Taasisi za nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) zimewasilisha maombi yao kwa Bunge la Afrika Mashariki na kupendekeza kusimamishwa uanachama nchi ya Burundi, ili kuilazimisha kushiriki mazungumzo ya Amani.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Chama cha Wanasheria wa Afrika (PALU),Donald Deya

Akiwasilisha maombi hayo jana Jijini hapa, mbele ya Kamati inayoshughulikia Usuluhishi wa Migogoro ya Bunge la Afrika Mashariki (EALA), Ofisa Mtendaji Mkuu wa Chama cha Wanasheria wa Afrika (PALU),Donald Deya, ametaka pia Burundi iwekewe vikwazo vya kiuchumi.

Amesema serikali ya Burundi imekuwa ikikataa kushiriki mazungumzo ya kutafuta amani nchini humo, kati yake na wapinzani huku machafuko na umwagaji damu, yakiendelea katika taifa hilo kutokana na mgogoro wa kisiasa.

Deya ambaye alikuwa akiwasilisha maombi hayo kwa niaba ya asasi na Taasisi hizo,amesema kutokana na kuongezeka kwa uvunjaji wa haki za binadamu nchini humo, nchi za Afrika Mashariki zinapaswa kuchukua hatua hizo, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kumaliza mgogoro huo.

Amesema wamefikia hatua hiyo baada ya kuona ripoti mbalimbali, zinaonyesha hali ya uvunjaji wa haki za binadamu, pamoja na mauaji ni mbaya na watu zaidi ya milioni moja ya wakimbizi wanazidi kuongezeka, hivyo ni wajibu wa Bunge hilo kuingilia kati, ili kuepusha umwagaji zaidi wa damu.

Pia amsema ni aibu kwa nchi za Afrika Mashariki, kufumbia macho suala hilo na zinatakiwa kuchukua hatua za haraka za kuokoa maisha ya watu nchini Burundi, la sivyo mauaji ya kimbari yanaweza kutokea nchini humo.