Jumatatu , 28th Sep , 2020

East Africa Radio kwa kushirikiana na duka kubwa la bidhaa la Jaden Home Store kupitia kipindi cha Mama Mia leo wameanza rasmi zoezi la kuwaongezea thamani Mama lishe bora Jijini Dar es Salaam kwa kuwapatia zawadi ya bidhaa mbalimbali zitakazowaongeza thamani kwenye biashara zao.

Moja kati ya wamiliki wa Jaden Home Store Jacqueline Maadili (kushoto) akimkabidhi TV ya kisasa mama lishe Yolanda Paul anayeuza chakula na vinywaji Ubungo Msewe ambayo itakakwenda kuongeza thamani katika biashara yake.

Mama lishe wa kwanza kabisa kuongezewa thamani kupitia mchakato huo East Africa Radio ni Yolanda Paul wa Divine Fast Food, iliyopo Ubungo Msewe, ambaye kutokana na mahitaji yake, amepatiwa Smart TV mpya kabisa ya kisasa kutoka Jaden Home Store ambapo anaeleza kuwa TV hiyo itasaidia kuwahabarisha pamoja na kuburudisha wateja wake wakati wakipata mlo.

Nilikuwa nahitaji kitu cha kuwavutia zaidi wateja wangu wanapo kula ili kuburudika, hivyo basi nikaona iwapo nitapata TV wateja wangu wataburudika wakati wa kipata mlo jambo ambalo litazidi kuniongezea wateja zaidi,” alisema Mama lishe Yolanda huku akishukuru.

Mama lishe wa pili kuongezewa thamani kupitia mchakato huu ni Sarah Moshi wa Mwenge Jijini Dar es Salaam, ambaye kutokana na mahitaji yake, amepatiwa Blender mpya kabisa ya kisasa kutoka Jaden Home Store ambaye anaelezea furaha yake kwa kuahidi kuitumia kutengeneza juisi safi itakayoongeza thamani kwenye biashara yake.

Sarah Moshi ni Mama Lishe kutoka Mwenge Jijini Dar es Salaam , akikabidhiwa Brenda mpya kabisa ya kisasa kutoka Jaden Home Store.

Moja kati ya wamiliki wa Jaden Home Store Jacqueline Maadili akikabidhi vifaa hivyo kwa Mama Lishe hao amewasihi kukuza biashara zao kwa kuwa wabunifu na kutokata tamaa kwa kuwa maisha ni mapambano.

"Ukimsaidia mwanamke mmoja umeisaidia jamii nzima, hicho ndicho kitu kilichotuhamasisha sisi Jaden Home Store kuungana na East Africa Radio kupitia kipindi cha Mama Mia ili kuongezea thamani Mama Lishe hawa,” alisema Jacqueline.